.

Saturday, May 14, 2011

SINDANO ZAWAUMBUA ARSERNAL.

PAUL Merson ameibua zengwe katika klabu ya Arsenal, baada ya kudai kwamba walikuwa wakidungwa sindano za dawa zisizojulikana kila wanapokabiliwa na mechi ngumu.
Nyota huyo wa zamani wa England, Merson, alisema hilo lilikuwa likitokea alipokuwa akikichezea kikosi hicho kinachonolewa na Mfaransa Arsene Wenger.
Katika mahojiano maalumu aliyofanya na jarida la soka la Ufaransa la So Foot, Merson alibainisha kwamba walikuwa wakifanyiwa mambo kama hayo walipokuwa Highbury.
Merson, 43, aliyecheza chini ya Wenger katika msimu wa 1996-97, alisema: “Wakati mwingine, katika mkesha wa mechi kubwa, tunakwenda kambini Holiday Inn huko Islington ambako tunadungwa sindano mikononi zenye dawa tusizozitambua.
“Sijawahi kuuliza swali lolote kuhusu hilo. Kwa kipindi kile tulikuwa tukimwamini kocha, unafanya kila kitu anachotaka wewe ufanye.”
Merson alibainisha kwamba hakujali kitu kwa sababu kwa kipindi hicho yeye binafsi alikuwa chapombe na mtumiaji mzuri wa dawa.
Aliongeza: “Kulingana ilivyokuwa utaratibu wa maisha yangu, ile sikuona ni tatizo kwangu na sikuhofia chochote.”
Merson alibainisha pia kila asubuhi wanapowasili kwenye uwanja wa mazoezi walikuwa wakipewa juisi ya machungwa iliyokuwa imechanganywa na ‘Creatine’.
Creatine inadaiwa kuongeza uwezo wa stamina kwa wachezaji na ndio maana ilikuwa ikitumiwa na Wenger kwa ajili ya wachezaji wake.
Merson, 43, alibainisha kila kitu walichokuwa wakifanya katika kambi ya timu hiyo ya Arsenal akibainisha kwamba wakati mwingine walikuwa wakipewa vidonge vikali vya caffeine kila wanapokwenda kucheza mechi za ligi za ugenini.
Katika kikosi hicho cha Arsenal, Merson alicheza zaidi ya mechi 400 na aliweka wazi hakuijua dawa ya njano iliyokuwa ikitumika kuwadunga kabla ya kushuka dimbani kumenyana kwenye mechi kubwa za Ligi Kuu.

MGANGA AJITOSA KWENYE UMISS.

WAKATI warembo 12 wanatarajiwa kushiriki katika shindano la kumsaka Miss Na Mwandishi
Bagamoyo, kwa upande mwingine limefanikiwa kumuibua mmoja kati ya madaktari wa tiba mbadala ya magonjwa mbalimbali, Dk. Kahenga.
Mashindano hayo ya Vodacom Miss Bagamoyo, yaliyoandaliwa na Asilia Decoration yanatarajiwa kufanyika Mei 28, mwaka huu.
Mratibu wa shindano hilo, Awetu Amir, alisema Dk. Kahenga mwenye sifa kubwa ya utabibu ni mmoja kati ya wadhamini wa shindano hilo.
Mbali na Dk. Kahenga wengine waliodhamini ni Kampuni ya Vodacom na Redds.
Awetu aliwaomba wadhamini wengine kujitokeza kwa wingi ili kufanya mashindano yawe na mvuto.

"NIACHENI NA YANGA YANGU JAMANI"

HATIMAYE mshambuliaji wa FK Jagodina ya Serbia, Mghana Kenneth Asamoah, ametua rasmi jijini Dar es Salaam  na kulakiwa na viongozi, wanachama na wapenzi wa Yanga kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Baada ya kutua kwenye uwanja huo, viongozi wa Yanga walikwenda naye moja kwa moja katika Makao Makuu yao yaliyopo katika makutano ya mitaa ya Jangwani na Twiga, jijini, kwa ajili ya kufanya naye mazungumzo ya mwisho ya kuichezea timu hiyo msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa.
Mchezaji huyo aliyeteka vichwa vya vyombo vya habari kwa siku za hivi karibuni hapa nchini, aliwasili saa 3:30 asubuhi.
Yanga ilijaribu kumsajili Assamoah kwa ajili ya msimu uliopita, lakini ilishindwa kumtumia kutokana na kukwama kwa Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) na hivyo kurejea katika klabu yake ya FC Jagodina, iliyomtoa kwa mkopo.
Na kutokana na kiwango alichokionyesha wakati wa mechi za maandalizi ya msimu uliopita, Yanga wameamua kumfuatilia tena ambapo Mghana huyo ameonyesha nia ya kukipiga Jangwani msimu ujao.
Lakini wakati Yanga wakiendelea na mchakato wao wa kumnasa Assamoah, hivi karibuni, watani wao wa jadi, Simba, walitangaza nia yao ya kuwania saini ya mshambuliaji huyo.
Wekundu wa Msimbazi hao, walifika mbali katika mchakato wao huo, wakidai kuwa jitihada zinazofanywa na Yanga, zitageuka kilio baada ya kufungwa kwa dirisha la usajili wa msimu ujao kwa kuwa watani wao hao wanatumia njia ya mkato.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Rage, aliwaambia waandishi wa habari katikati ya wiki hii kuwa wao wanamfuatilia Assamoah kwa kufuata sheria za Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), kuzungumza na klabu ya mchezaji kwanza badala ya kuanza na mchezaji kama wanavyofanya Yanga.
Rage alisema kuwa kinachofanywa na Yanga kinaweza kuigharimu klabu hiyo iwapo Jagodina watashitaki FIFA na mwisho wa siku, watani wao wa jadi hao, wataishia kunawa.
Kauli hiyo ya Rage ilionekana kuwachanganya wapenzi wa Yanga, wakihisi huenda klabu yao ‘ikaingia mkenge’ kwa Assamoah kama ilivyokuwa msimu uliopita.
Hatimaye jana Assamoah alikata mzizi wa fitina baada ya kutua Jangwani na kusema: “Nimekuja kulipa fadhila Yanga kwa kuwa msimu uliopita klabu hii ilionyesha upendo mkubwa kwangu.”
Alisema Yanga ni timu ambayo anaamini ina umoja na mshikamano, hivyo hiyo ni bahati kwake kuchezea timu hiyo na hayupo tayari kujiunga na timu yoyote nchini hata kwa uhamisho wa fedha nyingi.
Aliwaahidi mashabiki wa timu hiyo kuwa msimu ujao atahakikisha anarudisha ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Agosti, mwaka huu.
“Ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba nitajitahidi sana uwanjani kama ishara ya kuipenda timu yangu ya Yanga,” alisema Assamoah huku akionekana kuwa na furaha isiyo kifani.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga, alisema kuwa ni vigumu timu yoyote kumchukua mchezaji huyo, kwa kile alichodai kuwa bado wana makubaliano na timu anayochezea (Jagodina) kwa sasa.
“Kwa uwezo alionao Kenneth Assamoah, tuna mpango wa kumpa mkataba wa zaidi ya miaka mitatu,” alisema Nchunga.
Kenneth Asamoah, alizaliwa mwaka 1988 katika Mji wa Kumasi, nchini Ghana, ambapo mwaka 2006 alijiunga na Asante Kotoko ya huko na kuichezea kwa miaka miwili kabla ya kujiunga na FK Jagodina inayoshiriki Ligi Kuu ya Serbia ‘Super Liga’.

"MIMI NA SIMBA SC BASI"

OFISA Habari wa Simba, Clifford Ndimbo, ameachia ngazi kutokana na kile alichodai kutopata ushirikiano na uongozi wa klabu hiyo.
Ndimbo jana aliwasilisha barua ya uamuzi wake huo kwa uongozi wa klabu hiyo yenye maskani yake katika Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam.
Ndimbo bado alikuwa na mkataba na Simba, uliotarajiwa kumalizika Septemba mwaka huu.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Ndimbo alisema kuwa uamuzi huo ni wake binafsi na kwamba hajashawishiwa na mtu yeyote yule.
“Nashukuru kuwa nimefanya kazi nzuri wakati wa uongozi uliopita chini ya Mwenyekiti Hassan Dalali iliyopelekea uongozi wa sasa chini ya Mwenyekiti Ismail Rage kuhitaji kuendelea kupata huduma yangu,” alisema.
Ndimbo alisema: “Kwa kipindi chote ambacho nimekaa na uongozi uliopo madarakani, nimekuwa nikitekeleza majukumu yangu, japo wakati mwingine ni katika ugumu ambao nilipohoji, niliambiwa yote yatatatuliwa.”
Ndimbo alishawahi kuandika barua kama hiyo Aprili 5, mwaka huu na kujadiliwa na Kamati ya Utendaji ya Simba, kabla ya kuzuiliwa na Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Evodius Mtawala.
“Pamoja na uamuzi wake huo wa awali kuzuiliwa na Mtawala, hali ya kutoshirikishwa katika matukio ya klabu hiyo, iliendelea kama kawaida, ikiwamo Machi 28, mwaka huu, ambako katika kikao kilichofanyika Makao Makuu yao, hakushirikishwa na uongozi huo.
“Kudharauliwa na kutoshirikishwa…nimeonekana sina maana ndani ya Simba, hivyo uamuzi huu ni kutoka moyoni na somo kubwa kwangu,” alisema.
Wakati Ndimbo akitangaza kuachia ngazi, Ismail Rage alisema hana taarifa na kwamba yeye si mwajiri wake, bali ni Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Evodius Mtawala.
“Ni cheo kidogo sana cha Ndimbo, hivyo hakiniumizi kichwa na nilipowasiliana na Katibu kuhusiana na taarifa hizi, aliniambia hana taarifa,” alisema Rage.